tg

Wednesday, December 26, 2012

DC LUDEWA KUWAFIKISHA POLISI WAZAZI WANAOWALINDA MAFATAKI


Mkuu  wa  wilaya (DC) ya  Ludewa  mkoani  Njombe Juma Solomon  Madaha(pichani) amewataka  wazazi  wote  ambao  watoto  wao  wamechaguliwa  kujiunga na  elimu ya sekondari kuhakikisha  wanawapeleka   watoto  hao  kuanza masomo mapema  mwakani na atakayepuuza agizo  hilo atawajibishwa  kisheria pamoja na wazazi  wanaowalinda wanaume  wanaojihusisha na mahusiano ya kimapenzi na  wanafunzi (Mafataki).

Mkuu  huyo  wa  wilaya  ametoa kauli  hiyo leo  wakati  wa mahojiano maalum na mtandao  huu  wa www.francisgodwin.blogspot.com mjini Ludewa  kuhusu mkakati  wa wilaya  wa  katika  kusimamia elimu ya  sekondari   kwa   wale  waliochaguliwa  kujiunga na elimu  ya  sekondari .

 Madaha  alisema  kuwa  ili  kuhakikisha  kuwa  kila mtoto anapata  haki  yake ya msingi ya  kuendelea na masomo ni  vema kila mzazi  kuhakikisha anatimiza  wajibu  wake kwa  kumpeleka  mtoto  shule kama alivyochaguliwa  badala ya   kuwaruhusu  watoto  hao  kwenda  mijini  kufanya kazi  za ndani .

Hata  hivyo  alisema  kuwa  moja kati ya mkakati  wa  wilaya ya  Ludewa ni  kuhakikisha  watoto  wote  waliofaulu  kujiunga na  elimu ya  sekondari  wanaanza masomo mapema  zaidi na  kuwa moja kati ya  wajibu  wa mzazi  ni  kumpeleka  mtoto  shule.

Pia  alisema  kuwa  mbali ya  kuwabana  wazazi ambao  watashindwa  kusomesha  watoto wao  elimu ya sekondari pia  serikali ya  wilaya ya  Ludewa itawachukulia hatua kali  wale  wote ambao  watawakatisha masomo   wanafunzi  kwa  kuwapa mimba pamoja na  wazazi  watakaotetea  wanaume ambao  wamewapa mimba  watoto  wa  shule.

" Wapo baadhi ya  wanaume  ambao  wamekuwa na tabia ya  kuwarubuni  watoto  wa  shule kwa mapenzi na  kuishia kuwakatisha masomo kwa  kuwapa mimba  huku  wazazi  wakiwalinda  watu hao ambao  wanashindwa  kuwatafuta  akina asha Ngedere  kwa maana ya  wanawake  wenye umri  sawa na  wao na badala  yake  wamekuwa  wakikimbilia kufanya mapenzi na wanafunzi....nasema tutawabana wote na kuwafikisha  polisi"

Katika  hatua  nyingine  mkuu  huyo  wa  wilaya alisema  kuwa  wilaya ya  Ludewa  imeendelea na mkakati  wa  kuwalinda  watoto  wa  kike kwa  kuendelea na ujenzi  wa mabweni ili  kuwanusuru  watoto hao wa kike na vishawishi vya mapenzi  kutoka kwa  mafataki  hao.


Alisema  kuwa  utaratibu  huo wa  kujenga mabweni  utasaidia  kuwafanya  watoto  wa  kike  kusoma bila  kuwepo kwa  vishawishi  na kuwa  baadhi ya  wanafunzi  wamekuwa  wakishawishika na kuingia katika  vitendo  vya ngono kutokana na kuishi nyumba za kupanga na  kuishi mbali na  shule.

Aidha  alimpongeza mbunge  wa  jimbo la  Ludewa  Deo  Filikunjombe kwa jitihada  zake za kuendelea  kuwasaidia  watoto  yatima na  wale  wasiokuwa na uwezo  wa kwenda  sekondari  pamoja na kuchaguliwa  kujiunga na  elimu ya  sekondari.

Hivyo  kuwataka  madiwani  na maofisa   watendaji  wa kata na vijiji kuendelea  kuwajibika kwa  kufuatilia  maendeleo ya  watoto hao  .

Mbunge  wa  jimbo la Ludewa  Bw. Filikunjombe  alisema kuwa ofisi  yake  imekuwa na utaratibu wa   kusomesha   watoto 25 kwa   kila kata  kwa  kata  zote  zaidi ya 23  za  jimbo la  Ludewa na kuwa  moja kati  ya  sababu ya kufanya  hivyo ni  kuwasaidia  watoto hao  kupata  haki yao ya  elimu .

0 comments:

Post a Comment